Na Senior Libonge, Ulanga
WENGI wa wananchi walioshiriki katika mikutano miwili iliyofanyika katika kata za Lupiro na Itete, Iragua na Njiwa wilayani Ulanga, mkoani Morogoro ya kutoa maoni kwa tume ya mabadiliko ya katiba wametaka katiba mpya itoe haki ya wananchi kumiliki ardhi.
Wakizungumza katika mikutano hiyo iliyofanyika hivi karibuni, wananchi hao walisema kuwa kwa sasa ardhi ni mali ya serikali na rais ndiye mwenye mamlaka juu ya matumizi ya ardhi iliyopo nchini na kwamba ikiwa wananchi mmoja mmoja watamilikishwa ardhi na rasilimali zilizoko juu na chini ya ardhi hiyo zinaweza kutumika kama mtaji wa maendeleo.
Akitoa maoni yake katika mkutano uliofanyika kata ya Lupiro mkazi wa kata hiyo, Godfrey Cholwa, alisema kuwa ikiwa serikali itabaini katika ardhi kuna madini ni vema ikawalipa fidia wananchi kulingana na gharama za wakati husika.
“Lakini mara nyingi tumekuwa tukishuhudia wananchi wakiondolewa kwa nguvu kutoka kwenye maeneo yao na hata serikali inapolipa fidia hulipa kulingana na vigezo vya sheria ya zamani ambazo zimepitwa na wakati na havina tija kwa sasa,” alisema Cholwa.
Kwa upande wake, Rastic Mbise, alisema kuwa ikiwa katiba mpya itaweka umiliki wa ardhi chini ya wananchi wenyewe kutawawezesha kuitumia ardhi hiyo kama mtaji na kuitumia kupata mikopo kutoka taasisi mbalimbali za fedha ikiwa wananchi wataweza kupatiwa hati miliki.
“Ardhi ibakiye mikononi mwa wananchi ili kuepuka mikataba mibovu ambayo imeiingiza serikali yetu katika mivutano mikubwa na wananchi kufuatia baadhi ya wananchi kunyang’anywa ardhi yao na kupewa wawekezaji,” alisema.
Naye Abudul Said akichangia katika suala la umiliki wa ardhi, alisema kuwa ikiwa mwekezaji akitaka ardhi fulani kwa ajili ya shughuli za uwekezaji atapaswa kuwasiliana na mwananchi anayemiliki ardhi hiyo kisha kijiji na hali hiyo itaviwezesha vijiji kunufaika na rasilimali zilizoko katika vijiji vyao.
Hata hivyo, Miraji Daud, makazi wa kijiji cha Alabama katika kata ya Itete, Ayub Erick na Sixbetus Sengwila wakichangia maoni yao katika katiba mpya walisema kuwa umiliki wa ardhi ni vema ukawa chini ya serikali ya kijiji ili kuwanifaisha wananchi wa eneo husika.
“Ikiwa ardhi katika kijiji itabainika kuwa na raslimali kama madini serikali ya kijiji itaingia makataba na mwekezaji atakayehitaji kuchimba madini hayo na asilimia fulani ya mapato yatakayopatikana zibaki kijijini kwa ajili ya shughuli za maendeleo,” alisema Sengwila.
Katika hatua nyingine diwani wa kata ya Itete, Fotunatus Malunda, alipendekeza kuwa kiingizwe katika katiba kipengere kitakachowapa fursa wafungwa walioko gerezani na watanzania walioko nje ya nchi kuweza kupiga kura.
Malunda alidai kuwa katiba ya sasa inayabagua makundi hayo na hivyo kuwafanya watanzania hao kukosa haki yao ya msingi ya kupiga kura.
No comments:
Post a Comment